Buriani Luteni Jenerali Mayunga
KATI ya viongozi ambao
nilipenda kusikia kauli zao kuhusu Luteni Jenerali Silas Mayunga, aliyefariki
wiki iliyopita, Agosti 5, nchini India, ni Waziri wa zamani wa Ulinzi na Jeshi
la Kujenga Taifa, Kanali (mstaafu) Abdulrahman Kinana.
Kwa nini Kinana? Kwa
sababu anajua masuala ya jeshi katika sura mbili. Kwanza kama mwanajeshi; pili
Waziri wa Ulinzi. Lakini kubwa zaidi, anafahamiana kwa karibu na Mayunga.
Itakumbukwa Novemba mosi,
1978, majeshi ya aliyekuwa Rais wa Uganda, Idi Amin yalivamia Mkoa wa Kagera.
Uvamizi huo ulimsukuma Mwalimu Nyerere kuashiria ushindi kabla vita kuanza.
Nyerere aliashiria
ushindi kabla vita kuanza akisema; “sababu ya kumpiga tunayo, nia ya kumpiga
tunayo na uwezo wa kumpiga tunao.” Hakika, kauli hii ilihitaji si tu risasi za
kutosha, mizinga au makombora na silaha za kila aina kuisimamia, bali mashujaa
wa mstari wa mbele vitani.
Ilikuwa kazi kubwa, na
kwa kweli ilikuwa ni juu ya makamanda wa mstari wa mbele kuamua kuivunjia hadhi
kauli hiyo ya Amiri Jeshi Mkuu au kuisimamia kufa au kupona ili ibaki kuwa ya
ukweli.
Hivyo basi, ni kauli au
hotuba iliyopaswa kutetewa, kupiganiwa kufa au kupona ili kuuthibitishia
ulimwengu; Amiri Jeshi Mkuu -Rais Nyerere alikuwa sahihi kutangaza uwezo, nia
na sababu za kumpiga Amin upo.
Ingawa makamanda wa
mstari wa mbele walikuwa na zana za kivita, lakini hotuba ya Mwalimu
iliwaongezea silaha ya ziada ambayo ni uzalendo.
Miongoni mwa wapiganaji
waliotwikwa dhima hiyo nzito ni pamoja na Luteni Jenerali Silas Mayunga,
sambamba na wapiganaji wote wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na
Watanzania kwa ujumla, waliotoa ng’ombe hata kuku kulisha wapiganaji uwanja wa
mapambano.
Mstari wa mbele katika
uwanja wa vita, Luteni Jenerali Silas Mayunga na wenzake, kazi ilikuwa moja
tu-kufa au kupona ili kulinda si tu hadhi ya Tanzania, heshima ya wapenda haki
duniani.
Ni vita hii ya Kagera
ndiyo inayotajwa kumtambulisha zaidi Luteni Jenerali Mayunga ndani ya JWTZ na
Jeshi la Uganda. Vita hiyo ilimpambanua ni mpiganaji wa aina gani akiwa mstari
wa mbele.
Luteni Jenerali Mayunga ni nani?
Kama ilivyo kwa watu
wengi mashuhuri dunia, haikuwa rahisi kumtabiria mtoto mdogo aliyezaliwa Maswa,
Shinyanga, mwaka 1940; eti siku moja ataipigania nchi yake kufa au kupona,
akiwa katika uwanja wa mapambano ya risasi, mizinga na makombora mazito.
Bila shaka, hata
alipokuwa shuleni Bwiru Sekondari, Mwanza, walimu na wanafunzi wenzake
hawakujua unyeti wa Silas Mayunga nchini, miaka kadhaa iliyofuatia.
Pengine hata naye hakujua uzito wa uamuzi wake wa kuanza maisha
mapya ya kijeshi alipojiunga, na kwa mara ya kwanza na Jeshi la kikoloni, (Tanganyika
Rifles) Januari 10, mwaka 1963.
Safari yake kijeshi
imegusa nchi za Israel na Canada, akihitimu mafunzo ya kijeshi Julai 26, mwaka
1963 nchini Israeli na miaka 10 baadaye (1973), akafuzu kozi ya unadhimu na
ukamanda wa jeshi nchini Canada. Kozi ya Ukamanda wa Juu wa Jeshi alihitimu
mwaka 1974 nchini.
Juni 21, mwaka 1995, ni
siku ambayo Mayunga alijiwekea rekodi binafsi ya kushika cheo cha juu jeshini,
akipandishwa cheo kuwa Luteni Jenerali na miezi sita baadaye (Desemba 31, 1995)
alistaafu.
Mti mkavu akiwa jeshini
Mayunga ni kamanda
kiongozi. Amekuwa Mkurugenzi wa Mafunzo makao makuu ya jeshi, Kamanda wa
Brigedi ya 202 ya Tabora, na Kamanda wa Divisheni za 20 na 30 za Jeshi la
Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Huwezi kuzungumzia Operesheni Chakaza wakati wa
vita dhidi ya majeshi ya Idi Amin bila kumtaja kiongozi wa operesheni hiyo
ambaye ni Luteni Jenerali Mayunga.
Katika Operesheni Chakaza, Mayunga ndiye
aliyekuwa Kamanda wa Brigedi ya 206. Ndani ya Jeshi la Uganda Mayunga ana
historia muhimu. Amekuwa Kamanda wa Kikosi Maalumu cha JWTZ nchini Uganda kati
ya 1979 na 1980.
Lakini ukiondoa
pilikapilika za kijeshi, Mayunga amekuwa Mkuu wa Mkoa Singida mwaka 1977 –
1978, Balozi wa Tanzania nchini Nigeria mwaka 1989 hadi 1998 na Balozi wa
Tanzania katika Jamhuri ya Kidemokrasia Kongo (DRC) 1998 na 2002, alipostaafu.
Kinana na Mayunga Liberia
Kama nilivyoeleza awali,
nimezungumza na Kinana. Amekumbuka mengi kuanzia pilikapilika za kivita za
Mayunga akiongoza sekta ya Mbarara, sambamba na jukumu zito la kufundisha majeshi
ya Uganda ili si tu kusafisha masalia ya Idi Amin; bali kuliweka upya jeshi la
Uganda.
“Wakati ule (vita ya
Kagera) kulikuwa na sekta mbili. Sekta ya Masaka ikiongozwa na Musuguri na
sekta ya Mbarara akiongoza Mayunga,”
“Anazo sifa nyingi muhimu
kama kiongozi. Kwanza, uwezo wa kujichanganya na watu wote. Wanajeshi wote
walimpenda kama kiongozi, akiwa anaongoza vikosi vyote sekta ya Mbarara na
makao yao makuu yakiwa mji wa Mbarara -Uganda, hapo alikuwa akifundisha majeshi
ya Uganda.
“Nakumbuka pia mwaka
1994, nikiwa Waziri wa Ulinzi naye akiwa Balozi wetu katika nchi zote za Afrika
Magharibi, Umoja wa Mataifa ulituomba kupeleka wanajeshi wa kulinda amani
Liberia.
“Tulipeleka wanajeshi
1,000, nikiwa na Mayunga tuliwatembelea wanajeshi wetu kwa kweli aliwapa hotuba
nzuri sana ya kuhimiza uzalendo, wanajeshi wetu walifurahi kumwona na
kuzungumza na Mayunga wakitambua sifa yake ndani ya jeshi, akiwa vitani
Uganda,”
“Tulikuwa pale siku tano,
lakini kikubwa zaidi niligundua kuwa aliweza kuwa karibu sana na watu wa hizo
nchi alizokuwa akiiwakilisha Tanzania na hiyo ndiyo sifa yake kuu. Ni mtu wa
kuchanganyika na watu wote,” anaeleza Kinana.
Mayunga
Nimebahatika kuzungumza
na baadhi ya wapiganaji walioshiriki vita ya Kagera. Kwao, Mayunga ni mti mkavu
usiochimbwa dawa. Kwa mujibu wa simulizi zao, Mayunga alikuwa akiwajaza
uzalendo, ujasiri na kuwaondolea uchovu kila walipokuwa wakisonga mbele
kumkabili adui.
Kwa maelezo yao, Mayunga
ni mpiganaji aliyedhihirisha kuwa ushindi wa kivita hautokani na kigezo cha
silaha bora pekee, bali ni wapiganaji jasiri, wazalendo na hodari katika kupiga
hatua kusonga mbele na si hatua za kurudi nyuma-kumkimbia adui.
Huyo ndiye Mayunga ambaye
hakufa akiwa uwanja wa mapambano akihangaika kuikomboa nchi yake dhidi ya adui.
Ndiyo, hakufa kwa risasi, mizinga wala makombora ya adui vitani.
Pamoja naye, tunawaenzi
makamanda wetu waliofia vitani na waliorudi hai, walimsogeza adui nyuma na
kuyapa ushindi majeshi ya Tanzania na Watanzania.
Wapiganaji wote kuanzia vikosi vya nchi kavu, maji, anga na
intelijensia ya kijeshi (military intelligence) katika JWTZ na nchi kwa
ujumla, hatuna budi kusema; ingawa tumepoteza kamanda mwingine aliyesonga mbele
mstari wa mbele vitani, mwaka 1978 lakini tunaridhika ametimiza wajibu wake
kwetu, raia wenzake.
Ameishi kwa kutii mamlaka
ya nchi. Ameishi kwa kutii raia wenzake, ameishi kwa mujibu wa tamaduni za
Kitanzania. Huyu si kamanda wa kijeshi pekee, bali ni mpigania haki duniani.
Ingwa tunamlilia lakini tunaridhika, tunashukuru na kujipongeza
kwa kugonganisha ‘glass’ tukisema imewezekana, ametimiza
wajibu.
Ewe Luteni Jenerali
Mayunga, hakufa kwa risasi, mizinga wala milipuko yoyote pengine kama familia
yako ilivyohofia ukiwa vitani lakini sasa umekufa ukiwa kitandani ukitibiwa.
Buriani Kamanda Mayunga. Tunasikitika kwa kifo, lakini tunafurahi umetimiza
wajibu.
CHANZO:http://www.raiamwema.co.tz/
No comments:
Post a Comment